Na Mwandishi wetu.
Shahidi wa utetezi katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu, Brenda Rupia, amekubaliana na upande wa Serikali kwamba kuchoma vituo au karatasi za kupigia kura, kuharibu mali na hata kukata vidole vya waliopiga kura kunaweza kuzuia uchaguzi au kuwafanya wananchi wengine wasiingie katika mchakato wa kupiga kura.
Kauli hiyo ilitolewa jana Septemba 9, 2026, wakati Wakili wa Serikali Mkuu, Nassoro Katuga, akimhoji Brenda katika madodoso yaliyolenga kufafanua maana na athari za msimamo wa kuzuia uchaguzi uliokuwa ukihusishwa na Lissu na CHADEMA kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.
Katuga alimuuliza Brenda kuwa kama kuchoma vituo vya kupigia kura au kuchoma karatasi za kupigia kura kunaweza kuwa kitendo cha kuzuia uchaguzi, shahidi akajibu, “Ni sahihi.” Alipoulizwa kama kuharibu mali kunaweza kuvuruga amani na hivyo kusababisha kuzuia uchaguzi, Brenda pia alikubali. Aidha, alikubali kuwa kukata vidole vya watu waliopiga kura kunaweza kuwatisha wengine wasiende kupiga kura na hivyo kuzuia uchaguzi usifanyike.
Katika madodoso hayo, Katuga pia alimuuliza Brenda kuhusu haki ya vyama vingine kushiriki uchaguzi endapo CHADEMA inaamini katika demokrasia. Brenda alikubali kuwa vyama vingine vina haki kushiriki uchaguzi na kwamba hiyo ni haki ya kikatiba. Pia alikubali kuwa kumzuia mtu kushiriki uchaguzi si haki na kwamba kufanya hivyo ni kosa.
Hata hivyo, alipoulizwa kama anajua kwamba kumhamasisha mtu kuzuia uchaguzi ni kosa la jinai kisheria, Brenda alijibu, “Sijui kama ni kosa la jinai.” Katuga alipoendelea kumuuliza kama mtu aliyemsikiliza Lissu ana haki ya kuitafsiri hotuba yake kwa namna alivyoielewa, Brenda alikubali kuwa ni haki, akisema pia ni haki kwa mtu aliyeisikiliza na kuielewa hotuba kuifanyia kazi kwa namna anavyoona inafaa.
Katuga pia alimuuliza Brenda kuhusu kundi la wanachama 55 wa CHADEMA, maarufu G-55, ambao walikuwa wamepinga msimamo wa chama kuhusu kuzuia uchaguzi na kuuelezea kama uasi ambapo Brenda alikubali kuwa walikuwa wanachama wa CHADEMA na kwamba walipingana na msimamo huo. Alipoulizwa kama walipoona msimamo wa kuzuia uchaguzi unaashiria uasi walijitoa kwenye chama, Brenda alieleza kuwa waliendelea kubaki, lakini baadaye walijiondoa kwenye chama.
Katika hatua nyingine, Katuga alimuuliza kama baada ya G-55 kusema msimamo huo unaashiria uasi, Mwenyekiti alisema ni kweli msimamo huo unaashiria uasi. Brenda alijibu, “Ni sahihi.” Maswali hayo yaliibua moja kwa moja suala la namna msimamo wa kuzuia uchaguzi ulivyoeleweka na baadhi ya wanachama wa chama hicho wakati huo.













































